Upekee na Kanisa la Kristo
Makanisa ya Kristo (Warumi 16:16) kwa muda mrefu yamedhalilishwa kwa kusisitiza kwamba watu wote wanapaswa kumtii Mungu wa mbinguni, na kwamba utii huu unamaanisha kuwa watu hawapaswi kuchezea Neno la Mungu kwa kuanzisha makanisa mapya, mafundisho, kanuni, na dini zao wenyewe. Wamesisitiza kwamba,Biblia inaelezea kwa wanadamu kuhusu dini ya Mungu, yaani, Ukristo wa Agano Jipya. Ukatoliki, madhehebu ya Kiprotestanti, na wingi wa makanisa yaliyoanzishwa na wanadamu katika karne zilizopita ni kutoka katika “imani” (1 Timotheo 4:1).Wameendelea kusema kuwa inawezekana—na ni lazima—kwa mtu kurudi nyuma ya kanuni na uhusiano wa kimadhehebu, na kuwa Mkristo wa Agano Jipya pekee, mshiriki wa kanisa la Agano Jipya.
Msimamo huu wa kibiblia umewaletea wanachama wa makanisa ya Kristo mashambulizi mengi, dhihaka, na uhasama. Chuki hii hujitokeza katika shutuma kama: “Mnafikiri ninyi pekee ndiyo mnaokwenda mbinguni.” Hasa kutokana na mabadiliko makubwa ambayo yamefanyika katika utamaduni wa Marekani katika miaka 50 iliyopita, ambapo dhana ya “usalama wa kisiasa” na fikra za “Mimi niko sawa, Wewe uko sawa” zimeenea sana katika mawazo ya kitaifa, chochote kinachoonekana kuwa cha “kipekee” kinadharauliwa mara moja na kutupiliwa mbali kama “kutovumilia,” “kikatili,” “kinyume cha haki,” na hata “madhehebu ya siasa kali.” Mtazamo huu umeenea na kuathiri sehemu kubwa ya Wamarekani. Kwa mfano, zingatia kauli ifuatayo kuhusu jina la kanisa la Biblia:
Ukweli ni kwamba jina “Kanisa la Kristo” linabeba dhana ya mtazamo wa upekee kwa watu wengi katika utamaduni wetu. “Aaah, ndiyo,” mtu fulani atasema, “hawa ni wale watu wanaofikiri kuwa wao pekee ndio watakaoenda mbinguni.” Mwanamke mmoja alisema kwamba kamwe asingeingia katika jengo letu ikiwa angejua kuwa sisi ni “Kanisa la Kristo.” Hata hivyo, mara tu alipoingia na kuhisi uwepo wa Mungu katika mwili huu, hakuwa tayari kuondoka! Yeye na watoto wake—waliotoka katika madhehebu tofauti kabisa—wanajawa na furaha kwa kushiriki katika uzoefu wa Kristo ndani ya jamii hii ya imani (Shelly, 1998, msisitizo umeongezwa).
Je, ina maana gani kuwa na “mtazamo wa upekee”? Kamusi inafafanua neno “pekee” kuwa ni “kuondoa au kuelekea kuondoa; kutoruhusu kitu kingine; kisicholingana; kisichogawanywa au kushikiriwa na wengine; kisichoambatana na wengine; cha kipekee au cha pekee; kinachotenga baadhi au wengi, kama kutoka kwa uanachama au ushiriki” (American…, 2000, uk. 620).
Uchunguzi rahisi wa Agano Jipya unaonesha kwamba kanisa la Agano Jipya ni Kanisa la Kristo. Yeye mwenyewe alilijenga (Mathayo 16:18). Alijitoa kwa ajili yake (Waefeso 5:25) na alinunua kwa damu yake mwenyewe (Matendo 20:28). Analipenda, analilea, na anatamani kulihifadhi likiwa takatifu na lisilo na mawaa (Waefeso 5:25-27,29). Kanisa la Kristo halipaswi kulinganishwa na makanisa ya kimadhehebu ambayo yameanzishwa na wanadamu.
Hapa ndipo jina la kanisa linakuwa jambo muhimu. Kanisa la Kristo litavaa jina lake. Ni kweli kwamba kanisa linaweza kuvaa jina lake na kudai kuwa ni lake, ile hali kimsingi si lake. Lakini kanisa linalojiainisha kwa jina la kimadhehebu ambalo linapotosha umakini kutoka kwa Mwanzilishi wake (yaani, Kristo) kuelekea kwenye mafundisho fulani au kipengele kingine cha kiroho kilicho cha daraja la chini hakiwezi kusemwa kwa haki kuwa ni kanisa lake.
Ole wake ambaye, mantiki kama hiyo inakataliwa karibu kila mahali katika mazingira ya sasa ya uvumilivu usio na mipaka na kukubalika kwa kila kitu. Bila shaka, kupendekeza kwamba kuna “kanisa moja” (Waefeso 4:4a), na kwamba kila mtu mwenye uwezo wa kuwajibika analazimika kutii mpango wa wokovu wa Kristo ili aongezwe kwenye kanisa hilo moja, ni kuwa na “mtazamo wa upekee.” Hiyo ndiyo asili halisi ya ukweli;mtazamo huo ni finyu na unatenga.
Lakini je, kuna dalili nyingine mahali pengine katika Biblia zinazoonesha kwamba mapenzi ya Mungu ni ya kipekee? Je, Biblia inafundisha kwamba njia sahihi ya maisha na dini ni nyembamba, madhubuti, na yenye mipaka? Je, Biblia inaunga mkono mazingira ya sasa ya kuchukulia kila kitu kuwa ni sawa tu, kukubalika, na uwazi?
Fikiria tukio moja fupi la mfano. Mwanzoni mwa historia ya mwanadamu, Mungu aliwaweka mwanamume na mwanamke wa kwanza katika bustani nzuri ya paradiso. Aliwapa uhuru mpana wa kutumia hiari yao katika kufanya maamuzi ya kila siku kuhusu chakula (Mwanzo 2:16). Hata hivyo, aliwapa katazo moja: walilopaswa kujiepusha nalo la kula tunda kutoka katika mti fulani maalum (Mwanzo 2:17). Shetani alipinga katazo hilo na akamshawishi Hawa afanye vivyo hivyo (Mwanzo 3:4-5). Hawa alishawishika na kushindwa kuhimili tamaa za mwili wake, akala tunda lile, kisha akamshawishi mume wake kula pia. Matokeo yake Dhambi iliingia ulimwenguni, na familia ya kwanza ilibadilika milele na kufukuzwa kabisa kutoka katika bustani hiyo nzuri.
Swali: Je, katazo aliloweka Mungu kwa Adamu na Hawa lilikuwa la kipekee? Yaani, je, maagizo yake kwao “hayakuruhusu kitu kingine chochote? Je, maagizo ya Mungu yalikuwa “hayapatani” na kile ambacho Hawa alitaka kufanya? Je, amri ya Mungu “haikugawanywa au kushikiriwa na wengine”na “haikuambatana na mengine”? Je, mtazamo wa Mungu wa “fuata njia yangu au uondoke” ulikuwa haukubaliki? Kuuliza ni kujibu.
Fanya hesabu yako. Angalia tukio baada ya tukio, mfano baada ya mfano katika Biblia kutoka mwanzo hadi mwisho. Tumia maana ya neno “upekee” kwa kila kisa cha kibiblia ili kubaini ikiwa, kwa kweli, mahitaji ya Mungu ni ya kipekee.
Chunguza kesi za Kaini na Abeli (Mwanzo 4:1-8), Nuhu (Mwanzo 6:22), Ibrahimu (Mwanzo 26:5), Musa (Kutoka 17:6; Hesabu 20:7-12), Nadabu na Abihu (Mambo ya Walawi 10:1-3), Waisraeli (Hesabu 14:20-23; 21:4-9; Yoshua 6; 9:14; 1 Samweli 8), Eli (1 Samweli 3:13), Sauli (1 Samweli 13:11-14; 15), Mfalme Daudi (1 Samweli 21:1-6; 2 Samweli 11; 24), Uza (2 Samweli 6:6-7; 1 Mambo ya Nyakati 15:13), Yeroboamu (1 Wafalme 12:26-33), Samaria (2 Wafalme 17:7 na kuendelea; 18:12), Yosia (2 Wafalme 22:13 na kuendelea), Mfalme Uzia (2 Mambo ya Nyakati 26:16-21), Wayahudi waliorudi kutoka uhamishoni (Ezra 9-10), Anania na Safira (Matendo 5:1-11). Hitimisho lisiloweza kuepukika na lisilopingika kwa mtu mwenye moyo wa uaminifu ni kwamba maagizo ya Mungu kwa wanadamu daima yamekuwa ya kipekee.
Usifanye makosa: hakuna mwanadamu wala kanisa lolote lililo na “umiliki wa pekee wa kweli.” Wokovu wa Injili unapatikana kwa wote: “Kwa maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa”(Tito 2:11);“Na Roho na Bibi-arusi wasema, ‘Njoo!’ Naye asikiaye na aseme, ‘Njoo!’ Naye mwenye kiu na aje; na yeyote atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure” (Ufunuo 22:17).
Mungu ndiye anayeamua nani ataokolewa na nani atapotea. Hata hivyo, ametupa Neno Lake ili kutufahamisha mapenzi Yake na maamuzi Yake. Anasema kwamba anataka kila mtu aokolewe (1 Timotheo 2:4). Anasema pia kwamba hataki hata mmoja apotelee kuzimu (2 Petro 3:9). Lakini pia anasema kwamba watu wengi watatumia umilele wao kuzimu (Luka 13:23-24). Hakika Yeye ni mjumuishi kwa maana anatoa wokovu kwa wote bila upendeleo. Lakini pia Yeye ni mpekee kwa kuwa anahitaji mwitikio sahihi wa utiifu kwa maagizo Yake (Yohana 14:15).
Tutafanya vyema kuachana na wivu wetu mdogo mdogo, kiburi, na uaminifu wa kisiasa, tujitoe kujifunza mipaka sahihi ya maagizo ya Mungu, na kisha tujitahidi kufuata mapenzi Yake—“tukiiteka nyara kila fikira ipate kumtii Kristo” (2 Wakorintho 10:5). Yeye ni “mwanzilishi wa wokovu wa milele kwa wale wote wanaomtii” (Waebrania 5:9). Kuna njia mbili tu zinazowezekana maishani: “dhambi iletayo mauti, au utii uletao haki” (Warumi 6:16).
Yesu Mwenyewe alisema kwamba njia ya kwanza ya maisha ni “pana” na “wazi,” na kwamba watu wengi huchagua kwenda huko (Mathayo 7:13). Pia alitangaza kwamba njia ya pili ni “nyembamba” na “finyu” (yaani, ya kipekee!), na wachache tu huweza kujizuia kufuata njia hiyo ngumu na iliyonyooka (Mathayo 7:14; Luka 13:23-24). Wakristo waaminifu hawakatishwi tamaa wanapoitwa “wa kipekee,” kwa kuwa wao wanahubiri na kutetea kile ambacho Mungu Mwenyewe ameweka. Kwa hakika, uchunguzi wa kina wa Biblia unadhihirisha kwamba Yesu Mwenyewe alikuwa mtu wa upekee. Mungu, kwa kweli, ni Mungu wa upekee!
Marejeleo
American Heritage Dictionary of the English Language(2000), (Boston, MA: Houghton Mifflin), fourth edition.
Shelly, Rubel (1998), “What Is Your Church’s Name?” Lovelines, 24[5], February 4.
REPRODUCTION & DISCLAIMERS: We are happy to grant permission for this article to be reproduced in part or in its entirety, as long as our stipulations are observed.