KATIKA KRISTO
Mjadala mdogo sana upo kuhusu kile kilicho na uwezo wa kusamehe dhambi. Biblia iko wazi kabisa kwamba damu ya Kristo hudumisha sifa hiyo ya pekee. Mtume Paulo aliandika: “Katika yeye huyo (Kristo—KB), kwa damu yake, kuna ukombozi wetu, msamaha wa dhambi…” (Waefeso 1:7). Ingawa ni wachache wanaoweza kubishana na ukweli huu kwamba damu ya Yesu husamehe dhambi, bado kuna mkanganyiko fulani kuhusu mahali maalumu ambapo mtu huguswa na damu hiyo. Njia moja ya kujua wakati ambao mtu anapokutana na damu ya Kristo ni kuchunguza maneno “katika Kristo” katika Agano Jipya. Kulingana na toleo gani unasoma, neno “katika Kristo” linatumika takriban mara 80 tofauti.
Tunapata nini “katika Kristo?” Paulo katika kitabu cha Waefeso, alitumia maneno haya mara nyingi katika sura ya kwanza. Alisema kwamba “kila baraka ya rohoni” hupatikana katika Kristo (Waefeso 1:3). Pia alisema kwamba “msamaha wa dhambi” unapatikana katika Kristo pekee (mst. 7). Katika kitabu cha Warumi, alisema zaidi kwamba “ukombozi” (Warumi 3:24) na “uzima wa milele” (Warumi 6:23) vimo ndani ya Kristo. Mtume aliyevuviwa alimwambia kijana Timotheo kwamba “wokovu” uko katika Kristo (2 Timotheo 2:10). Ni wazi kwamba Paulo alitaka wasomaji wake waelewe kwamba kila kitu kizuri katika ulimwengu wa kiroho kinapatikana katika Kristo pekee. Alipokuwa akizungumzia mambo nje ya Kristo, Paulo alitoa picha mbaya ya mahali pasipo na tumaini na bila Mungu (Waefeso 2:12).
Baada ya kuangalia kishazi “katika Kristo,” swali linazuka: Mtu anaingiaje ndani ya Kristo? Inafurahisha kuona kwamba Agano Jipya linataja ubatizo wa maji kama kipengele kimojapo muhimu kinachomuweka mtu ndani ya Kristo. Warumi 6:3 inasema: “Au hamjui ya kuwa sisi sote tuliobatizwa katika Kristo Yesu tulibatizwa katika mauti yake?. Na Wagalatia 3:27 inatangaza: “Kwa maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo” (msis. uliongeza). Ingawa wengine wamejaribu kudai kimakosa kwamba ubatizo unaotajwa katika aya hizi mbili unarejelea ubatizo wa Roho Mtakatifu, watu wengi wa kidini hawajatumia njia hii mbaya ya kufikiri (Miller, 2003).
Andrew Davis, katika mchango wake kwenye kitabu cha: Why I Am A Baptist, aliandika kwamba ubatizo wa maji “uliamriwa na Kristo katika Agizo Kuu ( Mt. 28:19 ) na unaonesha maisha mapya katika Kristo kwa kila mfuasi ( Rum. 6)” (2001, uk. 118). Rejeo lake la Warumi 6 linaonesha kwamba anaelewa ubatizo wa maji unaojadiliwa katika sura hiyo. Conrad Mbewe aliandika: “Niliona pia kwamba ubatizo ulimaanisha kufa pamoja na Kristo, kuzikwa pamoja naye, na kufufuka pamoja naye katika upya wa uzima (Warumi 6:4). Ilikuwa ni onesho la nje la kimwili la uzoefu wa ndani wa kiroho” (2001, uk. 97). Kuhusiana na kifungu cha pili, Wagalatia 3:27, J. Newton Brown aliorodhesha Warumi 6:4 na Wagalatia 3:27-28 katika sehemu yake inayozungumzia ubatizo wa maji kama inavyofundishwa katika Agano Jipya (1994, ukurasa wa 23-24). .
Hebu, basi, tuweke vipande hivi pamoja. Ikiwa Biblia inasema kwamba msamaha na baraka zote za kiroho zimo ndani ya Kristo, na ikiwa Warumi 6:3 na Wagalatia 3:27 inaeleza waziwazi kwamba ubatizo wa maji ni hatua ambayo inamwezesha mtu kuingia ndani ya Kristo, basi mtu yeyote ambaye hajabatizwa kwa maji yupo nje ya Kristo. Maji ya ubatizo hayaokoi mtu yeyote yenyewe kama yalivyo, lakini ni mahali ambapo mtu huwasiliana na damu ya wokovu ya Kristo.
Inashangaza kwamba wakati huo huo vikundi vingi vya kidini na waalimu hufundisha kwamba Warumi 6:3 na Wagalatia 3:27 inarejelea ubatizo wa maji wakiwa wanakataa kwamba ubatizo wa maji unamweka mtu ndani ya Kristo. Msimamo kama huo unadhoofisha usomaji wa moja kwa moja wa vifungu hivi viwili, ambayo vinaonesha kwamba ubatizo wa maji ni hatua inayomwingiza mtu ndani ya Kristo na kuwasiliana na damu yake (kwa utafiti wa kina zaidi angalia Lyons and Butt, 2004).
Marejeleo
Lyons, Eric na Kyle Butt (2004), “Kuchukua Umiliki wa Kile ambacho Mungu Anataka: Uchunguzi Katika Wokovu,” [On-line], URL: https://www.apologeticspress.org/articles/2546.
Mbewe, Conrad (2001), “Kupeperusha Bendera Juu Barani Afrika: Tumaini la Kibaptisti kwa Bara Lililoharibiwa,” Why I Am a Baptist, ed. Tom Nettles na Russell Moore (Nashville, TN: Broadman & Holman).
Miller, Dave (2003), “Miujiza ya Kisasa, Kuzungumza-Lugha, na Ubatizo wa Roho Mtakatifu—Kukanusha,” [On-line], URL: https://www.apologeticspress.org/articles/2569.
Brown, J. Newton (1994), Mwongozo wa Kanisa la Kibaptisti (Valley Forge, PA: Judson).
Davis, Andrew (2001), “Hisi Zetu Zinapoingia Njiani: Kutokana na Sakramenti za Kikatoliki hadi Usadikisho wa Wabaptisti,” Kwa Nini Mimi ni Mbaptisti, ed. Tom Nettles na Russell Moore (Nashville, TN: Broadman & Holman).
REPRODUCTION & DISCLAIMERS: We are happy to grant permission for this article to be reproduced in part or in its entirety, as long as our stipulations are observed.